JE, UKAWA UTASHINDA KAMA APC NIGERIA?



Umoja Wa Katiba ya Wananchi (UKAWA) ni umoja ulioanzishwa na baadhi ya vyama pinzani nchini Tanzania vikiwemo CHADEMA, NCCR, CUF na vingine.

Umoja huo unafanana na umoja ulioundwa na vyama vikuu vitatu vya upinzani nchini Nigeria ambavyo viliungana mnamo mwaka 2013 ambavyo ni Action Congress of Nigeria (ACN), the Congress for Progressive Change (CPC), the All Nigeria Peoples Party (ANPP) ,All Progressives Grand Alliance (APGA) na kuunda umoja unaoitwa All Progressive Congress (APC) ambao ulimpa ushindi Rais Muhammadu Buhari dhidi ya aliyekuwa rais Goodluck Jonathan.

Lengo la umoja huo ni kuunganisha nguvu za wanachama wa vyama hivyo ambao watakuwa na nguvu moja hata katika kupiga kura utakapofika uchaguzi mkuu mwezi September mwaka huu.

LOWASA KUJIUNGA UKAWA
Wachambuzi wa mambo wanasema umoja huo umeongeza nguvu zaidi hasa baada ya hapo jana tarehe 28 Agosti mmoja kati ya kada mkubwa wa CCM na aliyewahi kuwa waziri mkuu Edward Lowasa kujiunga na CHADEMA ambacho kipo chini ya mwavuli wa UKAWA.

Kujiunga kwa Lowasa kunatajwa kuwa huenda yakawa mafanikio makubwa kwa kuwa ana wafuasi ambao watalazimika kumfuata na kuunga mkono juhudi za UKAWA kukiangusha chama tawala.
Kuhama huko kwa Edward Lowasa kunatajwa kuwa ni kutokana na jina lake kukatwa katika listi ya watia nia kupitia Chama Cha Mapinduzi jambo ambalo kwa upande wake aliliona kama ni kukatiza ndoto zake za kuwa  Rais.

Muungano wa UKAWA unafanana na Muungano wa nchini Nigeria uliowafanya wapiga kura wa vyama hivyo tofauti vilivyoungana kumpigia kura mgombea mmoja aliyesimamishwa kugombea na hiki ndicho wanachokilenga UKAWA kwa kuangalia mtu anayekubalika katika eneo husika na kumsimamisha kuwa mgombea.

Umoja huo unaongeza nguvu kwa vyama pinzani kwa maana ya kwamba mgombea atakayeteuliwa na umoja huo atapigiwa kura na wanachama wa vyama vyote vinavyounda umoja huo.
Tumeshuhudia katika uchaguzi wa serikali za mitaa mwezi wa 12 mwaka 2014 upinzani ulipata viti vingi kuliko miaka ya nyuma hivyo hii inaweza kutafsiriwa kuwa Muungano wao kwa jina la UKAWA ulifanikisha kuongeza nafasi ya ushindi.

UKAWA ulianzishwa mnamo mwaka 2014 wakati wa mchakato wa kuchambua na kupitia rasimu ya katiba iliyowasilishwa na Mwenyekiti wa tume ya Rasmu ya katiba iliyopewa jukumu ukusanyaji wa maoni  juu ya katiba mpya Jaji Sinde Joseph Warioba.

Kutofautiana itikadi na mawazo kati ya wawakilishi waliochaguliwa kujadili rasimu hiyo ambao wengi wao ni wabunge na watu kutoka taasisi mbalimbali kulipelekea baadhi ya  wawakilishi na wabunge kutoka vyama pinzani kususia mchakato huo na kudai kuwa umechakachuliwa kwa kuondoa baadhi ya maoni ya wananchi.
Tukirudi Nigeria Umoja wa APC ndio ulimpa ushindi Muhammadu Buhari na kuwa Rais wa Nigeria baada ya kumuangusha Rais Goodluck Jonathan wa chama tawala cha PDP hivyo swali lililopo ni je, nguvu ya UKAWA itaweza kukiondoa Chama Cha Mapinduzi?
By Benezeth Kahwa
0766522469

No comments